MWENYEKITI wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Mstaafu Joseph Warioba amesema moja ya mambo yaliyohojiwa na wananchi wengi katika mchakato wa kukusanya maoni ya Katiba Mpya ni mfumo wa uongozi na utawala, hasa mamlaka ya uteuzi.
Amesema katika mikutano ya ukusanyaji huo wa maoni iliyofanyika katika mikoa saba ikiwamo Kusini Unguja na Kusini Pemba, wananchi walihoji madaraka aliyonayo Rais katika uteuzi wa nafasi mbalimbali zikiwamo za watendaji wakuu wa taasisi za Serikali.
Kauli hiyo imekuja wakati Tume hiyo ikiwa imemaliza awamu yake ya kwanza ya kukusanya maoni ya wananchi huku ikitarajia kuendelea tena na zoezi hilo katika mikoa mingine saba, kuanzia Agosti 26 mwaka huu.
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Jaji Warioba alisema wananchi 188,679 walihudhuria mikutano ya Tume kati yao 46,620 walitoa maoni yao.
Alisema watu 17,440 walitoa maoni kwa njia ya kuzungumza na 29,180 kwa njia ya maandishi.
Alisema katika mikutano hiyo wananchi walihoji masuala mbalimbali likiwamo la mfumo wa uongozi na utawala wakielekeza katika kutaka mabadiliko katika utezi wa wakuu wa mikoa, wilaya na watendaji wengine wa Serikali.
“Wananchi walihoji uteuzi wa nafasi mbalimbali ndani ya Serikali likiwemo suala la uteuzi wa wakuu wa mikoa, wilaya na watendaji wengine wa Serikali,” alisema Jaji Warioba na kuongeza;
“Wananchi wameonyesha wazi kwamba wanataka Katiba ya aina gani, wana uelewa mkubwa kuhusu maisha yao kuliko tunavyodhani, hata wasomi nchini wanatakiwa kutambua wazi kwamba, wakitaka kujua wanachokitaka Watanzania waende vijijini kuwasikiliza wananchi.”
Kwa mujibu wa katiba iliyopo wakuu wa mikoa, wilaya na watendaji wengine wa juu wa Serikali wakiwamo jaji mkuu, wakuu wa mashirika na taasisi nyeti za Serikali utezi wake hufanywa na Rais.
Alisema kuwa mambo mengine ambayo wananchi hao walitaka yaingizwe katika Katiba Mpya ni pamoja na masuala ya ardhi, kilimo, elimu, huduma za afya, hifadhi za jamii, nafasi ya utoaji wa haki na madaraka ya wananchi.
Alisema kuwa licha ya kuwa Watanzania wengi hawaijui Katiba ya sasa, lakini maoni waliyoyatoa yanaendana na vifungu vilivyomo katika Katiba hiyo.
Alifafanua kwamba licha ya kuwa muda wa miezi 18 ambayo imepewa tume hiyo kuwa mdogo, ni lazima tume hiyo ifanye kazi kwa umakini ili uchaguzi wa mwaka 2015 ufanyike huku kukiwa na Katiba Mpya.
“Tunapenda sana uchaguzi wa 2015 ufanyike wakati nchi ikiwa na Katiba Mpya na lazima tufanye kazi hii ndani ya muda uliopangwa” alisema Jaji Warioba.
Onyo
Katika hatua nyingine, Jaji Warioba alivitaka vyama vya siasa, mashirika ya dini, wanaharakati na asasi za kiraia kuacha kuingilia uhuru wa wananchi kutoa maoni kwa kuwataka wafuate misimamo ya vyama, taasisi na asasi zao.
Jaji Warioba alitumia mkutano huo kuzitaka asasi za kiraia, vyama vya siasa, wanaharakati na mashirika ya dini kuacha tabia ya kuwaelekeza wananchi cha kuzungumza wakati wakitoa maoni.
Alisema sheria ipo wazi kwamba makundi hayo yakitaka kutoa elimu kwa wananchi yanatakiwa kutoa taarifa kwa Tume, huku akisisitiza kuwa hata vikipewa nafasi hiyo viitumie vyema na sio hiyo kuwapangia wananchi cha kuzungumza.
Aliongeza kuwa kutokana na waumini wa dini ya kiislamu kuwa katika mfungo wa mwezi Mtukufu wa Ramadhani, kuwepo kwa sensa ya watu na makazi, tume hiyo imeamua kusogeza mbele tarehe ya ukusanyaji wa maoni, itaendelea na zoezi hilo kuanzia Agosti 26 mwaka huu.
Alisema mikoa ambayo Tume itakwenda kukusanya maoni ya wananchi katika awamu hii ya pili ni Lindi, Mwanza, Kigoma, Mbeya, Katavi, Morogoro na Ruvuma.
Katika awamu ya kwanza Tume hiyo ilikusanya maoni katika mikoa ya Pwani, Dodoma, Manyara, Kagera, Shinyanga, Tanga, Kusini Unguja na Kusini Pemba.
WARIOBA; Wananchi wanahoji mamlaka ya Rais
Jitokezedirectory
Friday, August 10, 2012
Popular Posts
-
NEW YORK, Marekani VIDEO iliyoonyweshwa mwishoni mwa wiki katika mitandao mbalimbali ya kijamii, ambayo ilielezea madhara ya taratibu ana...
-
RAIS Jakaya Kikwete ameeleza mikakati ya Serikali yake kuwa ni kuhakikisha inamaliza kabisa maambukizi mapya ya virusi vya Ukimwi ifikapo...
-
Uingereza imesitisha kwa muda msaada iliyokuwa iipe Rwanda kwa sababu ya wasiwasi kuhusu kuhusika kwa nchi hiyo katika mzozo uliopo Jam...
-
BAADA ya juzi Jeshi la Polisi kuwahoji na kuwaachulia huru wabunge wa Chadema, jana asubuhi walikamatwa na kutupwa korokoroni hadi kesho ...
-
Huduma ya Maji na Nishati (EWURA), Mhandisi Godwin Samwel, akizungumza na wanahabari jana jijini, Dar es Salaam kuhusu kupanda kwa bei za m...
-
HERIETH MAKWETTA MSANII wa muziki wa kizazi kipya kutoka Tanzania, Rehema Chalamila maarufu kama Ray C, yupo katika kituo maalumu cha msa...
-
MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu imewasafisha aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Italia, Profesa Costa Mahalu na Ofisa Utawala wa ubalozi ...
-
UPELELEZI wa kesi inayomkabili Msanii wa filamu nchini, Elizabeth Michael maarufu kama Lulu, anayekabiliwa na kesi ya mauaji katika Maha...
-
Wananchi wameshauriwa kutekeleza agizo la Utalii kwa wote kwa kuyatembelea maeneo mbali mbali ya utalii Zanzibar ili kufahamu historia y...
-
KUTOKANA na kile kichoonekana ni kutaka kukabiliana na uhaba wa sukari na kupanda kwa bei yake, Waziri Mkuu Mizengo Pinda anatarajia kukuta...
Habari Leo Tanzania, Media, (East Africa)
0 comments:
Post a Comment